MBINU ZA KUSHINDA MASWALI YA USAILI WA KAZI
MBINU ZA KUSHINDA MASWALI YA USAILI WA KAZI
Mwl. Juma
Baruapepe: jumapeter399@gmail.com
Rununu:
+255762957992
Sehemu kubwa ya usaili ni maswali
na majibu yanayolenga kupima uwezo wako wa kukabiliana na changamoto halisi za
kazi. Ingawa yapo maswali yanayoweza kukupatia wasiwasi wa nia ya mwuulizaji,
fahamu kuwa hakuna swali linaulizwa kwa nia mbaya au kwa bahati mbaya.
Kila swali linaloulizwa linalenga
kutafuta uthibitisho kuwa wewe ni mtu sahihi wa kazi unayoomba.
Vijana wengi wenye ufaulu mzuri
kitaaluma wanaoomba kazi hujikuta pasipokujua wakifanya makosa madogo
yanayowagharimu. Kwa kuwa umetumia muda wako kuandika barua, kuandika wasifu
wako binafsi wa kazi, wakati mwingine kusafiri kwenda kuhudhuria usaili, ni
muhimu kufanya maandalizi yatakayokuongezea nafasi ya kufanikiwa.
Katika makala haya, tutaangazia
baadhi ya maswali yanayoulizwa kwenye usaili wa kazi na namna unavyoweza
kuyajibu.
1.Mapokezi
Unapokaribisha kwenye usaili,
jambo la kwanza ni kuhakikisha kuwa unatengeneza taswira ya mtu anayejitambua,
mkomavu na mwenye nidhamu. Salimia jopo linalokupokea kwa tabasamu na salamu ya
adabu yenye kuonesha kujiamini. Ikiwa ni lazima kushikana mikono na wanajopo
fanya hivyo kwa kujiamini.
Kisha, kuwa mtulivu uelekezwe mahali pa kukaa. Hakuna sababu ya kuwa na
papara kukaa mahali hata kama unahisi ndiyo sehemu iliyoandaliwa kwa ajili
yako. Unapokaa, kaa mkao unaoashiria mtu mnyenyekevu asiye na makuu.
Mara nyingi kukaa wima ni vizuri na kuambatane na hali inayoonesha kuwa
unayo motisha ya kupata kazi unayoomba.
Kunja miguu yako kistaarabu ukikutanisha mikono yako juu ya mapaja kutuma
ujumbe wa mtu mtulivu. Egemea mbele badala ya nyuma, watazame wanajopo machoni.
Kwa haraka, wazoee wanajopo kwa kuwaona ni watu wa kawaida lakini
wanaostahili heshima.
Unapojibu maswali, epuka kutikisa kichwa. Kukunja nne, kuegemea nyuma au
kuweka mikono kwa namna inayoonesha mamlaka ni kutuma ujumbe hasi usiokusudiwa.
2.Utambulisho
Kumbuka kuwa usaili wako ulianza
tangu jopo la usaili lilipopokea nyaraka zako. Kwa kiasi fulani, tayari wanayo
taswira fulani kukuhusu. Una kazi muhimu ya kuwathibitishia kuwa hayo
uliyoyaandika yana ukweli.
Mara nyingi unapokaribishwa
kwenye usaili, kiongozi wa jopo la usaili atawatambulisha wenzake. Anapofanya
hivyo, ana lengo la kukufanya uwazoee wanajopo, utulie na usiwe na wasiwasi.
Shukuru kwa utambulisho wao.
Kiongozi huyo anaweza kukutambulisha wewe kwa jina lako na kukukaribisha
maswali. Mara nyingi swali linaloanza ni “Tuambie
wewe ni nani? Karibu ujitambulishe”
Swali kama hili halihitaji utaje majina yako bali kufahamu muhtasari wako
kikazi. Ingawa utakayoyasema yatatokana na uliyoyaandika kwenye wasifu wako wa
kazi, mara nyingi hautarajiwi kurudia maelezo hayo.
Jipambanue wasifu wako kikazi na kiutendaji. Jopo linatarajia uwaambie
mambo ya msingi unayoyaamini yanaweza kuwasaidia kuelewa mtazamo wako kikazi.
Ongelea majukumu ya kikazi uliyowahi kuyafanya ukiyaoanisha na kazi unayoiomba.
Anza na kazi ya nyuma zaidi ukimalizia na kazi unayoifanya sasa hivi au ya hivi
karibuni zaidi.
3.Ari na uwezo wako wa kazi
Unaweza kuulizwa “Kwanini unafikiri
tukuchukue kwa nafasi hii? Kwanini unataka kufanya kazi na sisi?” Watu
wengi wanapoulizwa swali hili hufikiri wanachohitaji ni kujilinganisha na
wengine kwa majina. Huna sababu ya kuwataja wengine kama namna ya kuonesha
unavyofaa zaidi.
Kwa swali kama hilo, kimsingi wanataka kuona kama unaielewa taasisi yao.
Thibitisha kuwa umeitafiti taasisi kwa kina na uelewa wa huduma wanazozitoa.
Onesha unavyojisikia kuwa sehemu ya malengo mapana ya taasisi yao.
Kadhalika, ni fursa kwako kuonesha namna gani vipaji na ujuzi ulivyonavyo
vinaweza kumsaidia mwajiri wako mtarajiwa. Lijibu kwa ujasiri bila kusita.
Ukionesha wasiwasi katika majibu yako, wanaokusaili nao watakuwa na wasiwasi na
uwezo wako.
Onesha namna gani unafaa kuajiriwa kwa sababu ya uwezo wako.
Katika eneo la ari na uwezo wako wa kazi, unaweza kuulizwa “Unafikiri utaongeza tija gani katika taasisi
yetu?”
Hapa ongelea ujuzi na uzoefu wa kazi unaofikiri unaweza kumsaidia mwajiri wako
kutatua changamoto alizonazo.
Jitahidi kuonesha namna ujuzi na vipaji ulivyonavyo vinavyoweza kutumika
katika maeneo mengine zaidi ya nafasi uliyoomba. Kwa kawaida, mwajiri huvutiwa
na mtu anayeweza kutumika katika eneo zaidi ya moja.
Pia unaweza kuulizwa “Unaweza
kuniambia mapungufu uliyonayo?” Usiwarahisishie kazi ya kuyaelewa mapungufu
yako waziwazi. Waache wao wenyewe wayajue. Badala yake zungumzia mapungufu
ambayo mtu akiyatafakari anaona ni tija.
Mfano, “napenda kufanya kazi muda mrefu,
napenda kufanya mambo kwa ukamilifu kiasi cha kujikuta sina muda wa kutosha
kukamilisha kazi kwa wakati ninaotaka”
4.Uzoefu wako huko ulikotoka
Unaweza kuulizwa maswali mengi kuhusu uzoefu wako kazini. Ikiwa kwenye
wasifu wako wa kazi ulionesha kuwa uliwahi kufanya kazi mahali na ukaiacha,
unaweza kuulizwa swali “Kwanini uliacha
kazi yako? Au kwanini unataka kuacha kazi uliyonayo?”
Hili ni swali gumu. Mwuulizaji analenga kupima uaminifu wako na anataka
kujua mambo gani hasa yanakuridhisha kazini. Kimsingi, lengo siyo kujua
yalitofanyika huko uliko (kuwa) bali kujua unavyoweza kumfaa. Hutakiwi
kuzunguka kwa kutafuta sababu zisizo za ukweli. Jibu kwa urahisi na uwazi
lakini ukiwa makini.
5.Matarajio yako kwa mwajiri
“Unafikiri tukulipe mshahara kiasi
gani?”
Hili swali linatafuta kujua vipaumbele vyako uwapo kazini. Ni kweli
unatafuta kazi ili upate fedha uboreshe maisha yako. Lakini kuonesha kuwa ari
na kujituma kwako kazini kunategemea kiasi cha pesa unacholipwa ni kosa la
kiufundi. Kosa hili linaweza kuwa kikwazo cha kupata kazi.
Unatakiwa kuonesha ukomavu kwa kuelewa kuwa taasisi bora kama hiyo
unayotaka ikuajiri zina utaratibu rasmi wa kuwalipa wafanyakazi wake. Mtu
hulipwa kwa sifa alizonazo. Kwa uelewa huo utapata alama za ziada.
Hata hivyo, pamoja na majibu hayo wapo wasaili wanaweza kukubana uwaambie
matarajio yako. Fahamu kuwa kujadili mshahara wa kazi ambayo bado hauna uhakika
nayo haiwezi kukusaidia.
Ikiwa utalazimika kutaja tarakimu, inatarajiwa kuwa tayari utakuwa umefanya
utafiti wa taasisi hiyo ikiwa ni pamoja na viwango vya mishahara. Taja kiwango
ambacho hakitaonesha huna thamani lakini pia usitaje kiwango kitakachoonesha
kujikweza kupita kiasi.
6.Uelewa wa mambo na ujuzi wa
kazi
Unaweza kuulizwa maswali yanayopima uelewa wako wa kawaida kwa mambo
yanayofahamika. Lakini pia unaweza kuulizwa masuala ya moja kwa moja
yanayohusiana na kazi unayoomba.
Wakati mwingine, baadhi ya wasaili hutumia mtihani wa kuandika kujaribu
kuthibitisha kama kweli una uwezo na ujuzi uliouonesha kwenye wasifu wa kazi.
Maswali yanayoulizwa yanaweza kupima moja kwa moja utaalamu uliousomea
darasani au namna unavyoweza kutatua changamoto halisi za kazi. Jiandae
ipasavyo kwenye maeneo muhimu.
Kilicho muhimu ni namna unavyoweza kutafsiri nadharia katika mazingira ya kazi.
Kwa mfano, unaomba kazi ya uhasibu msaili mmoja anakuuliza “Chukulia ofisini kwako kumetokea wizi wa
fedha. Utachukua hatua gani? Au unaomba kazi inayohusika na utawala “Chukulia kama kiongozi umesikia wafanyakazi
wa chini yako wana mpango wa kugoma, utafanyaje?”
Hayo ni maswali ya uchokozi. Usitumie muda mrefu kutafuta masuluhisho
yasiyokuwepo. Jibu kwa ujasiri kuwa hutarajii kuwa matatizo ya namna hiyo
yatajitokeza. Lengo ni kuonesha una uwezo wa kuikinga taasisi yako na
changamoto kama hizo.
7.Malengo yako ya baadae
“Unajiona ukifanya nini baada ya
miaka 10 ijayo? Una malengo gani ndani ya miaka mitano ijayo?”
Hapa unahitajika kuonesha ari ya kukua kiujuzi na kiweledi. Ongelea mipango
ya kujifunza zaidi kufikia kwenye malengo makubwa yanayoendana na malengo ya
mapana ya kitaasisi. Kuzungumzia malengo yasiyoendana na kazi unayoomba
kutakupunguzia alama.
“Umeomba kazi kwingine?” Wanahitaji
kuwa na uhakika na maamuzi yako. Ni kweli inawezekana utakuwa umeomba kazi
maeneo mengine. Lakini utaonekana mkomavu ukiweza kuonesha kuwa kazi hii
unayosailiwa ndio chaguo la kwanza.
“Utafanya kazi na sisi kwa muda gani?” Hapa wanataka kujua kama wewe ni
mpitaji tu au la. Inawezekana kweli unaweza kuwa na mpango wa kufanya kazi kwa
muda mfupi na utafute njia nyingine.
Lakini kuonesha wazi kuwa unapita wakati hata kazi hujapata si busara.
Onesha ungependa kufanya kazi kwa muda mrefu kadri utakavyohitajika.
“Unaota kufanya kazi gani baadae?” Ukitaja kazi nyingine mbali na hiyo
unayoomba, unaleta wasiwasi kuwa hutoridhika na kazi unayoomba.
Ongelea mazingira ya kazi bila kutaja kazi mahususi. Mfano, kazi
inayokufanya utumie vipaji vyako na ujuzi ulionao. Kazi inayokufanya ukue
kiujuzi na kiuzoefu.
“Uko tayari kuanza kazi lini?” Kama huna kazi ukisema uko tayari kuanza kazi
mara moja inaonesha utayari ulionao. Lakini kama unabadilisha kazi kuonesha
utahitaji muda mfupi wa kukamilisha taratibu za kukabidhi majukumu uliyonayo na
kuaga itakupatia alama.
8.Fursa ya kuuliza swali
Kwa kawaida, baada ya kuulizwa maswali mengi, kikao cha usaili
kitahitimishwa kwa kukukaribisha kuuliza swali. Kama tulivyosema, kila swali
lina maana kwenye usaili.
Unapoulizwa “Je, una swali ungependa
kuuliza?” Lengo ni kutaka kujua ulivyo na ari ya kufanya kazi na taasisi
hiyo.
Usipouliza swali lolote, maana yake ama huna uelewa wa mambo mengi au huna
ari ya kutosha. Uliza swali kuhusu taasisi hiyo. Waulize wanatarajia nini kwa
mtu atakayepata kazi hiyo.
Kadhalika, waweza kuulizia mambo yanayohusiana na fursa wanazoweza kutoa
kukuza ujuzi wako kama mfanyakazi wao.
Epuka kuuliza maswali ya kimaslahi. Kuuliza “Mnanilipa bei gani?” ni kuonesha huna mtazamo mpana na kazi.
Unaweza hata usijibiwe au ukajibiwa jibu litakalokunyong’onyeza.
Ahsante.
No comments