IKIRARI  NA HAKIMILIKI

Mimi JUMA PETER ninathibitisha kwamba mashairi haya ni yangu, na kwamba sijanakili wala kulahamu kwa namna yoyote ile, na hayajawahi kuwasilishwa wala hayatawasilishwa katika chuo kikuu kingine chochote kwa ajili ya kukidhi matakwa ya kitaaluma ya kozi za ubunifu na utunzi wa kazi bunilizi za kifasihi.
Haki zote zimehifadhiwa. Hairuhusiwi kuzalisha, kuiga, kunakili, kutafsiri, kupiga chapa kwa namna yoyote iwayo wala kusambaza sehemu yoyote ya mashairi haya kwa namna yoyote ile bila kibali cha maandishi kutoka kwa mwandishi.

ANUANI YA MTUNZI:
Mwl. Juma Peter
S.L.P 1226
Moshi-Tanzania
Rununu: +255762957992
ISBN: 978-9976-5318-0-7
Sehemu ya matini tepe hii ya mashairi yanapatikana katika kitabu change cha mashairi kiitwacho JICHO LA KURUNZI kimechapwa na:
 Beanna Printing Solutions
Morogoro Tanzania
+255766770422, +255713360853

 


SHUKURANI

Namshukuru Mungu wa Mbinguni aliyenipatia ujasiri na mawazo ya kutunga mashairi jina la Mwenyezi Mungu muweza wa yote lihimidiwe.
Nawashukuru walimu wangu wote kwa kunifundisha katika ngazi tofauti tofauti za Elimu na taaluma kuanzia Elimu ya Msingi hadi Chuo Kikuu. Napenda kuwashukuru wahadhiri wangu wa kozi za Fasihi na Isimu wa Chuo Kikuu Cha Kikatoliki Mwenge kilichopo Moshi-Kilimanjaro kwa moyo wao wa dhati kunielekeza mambo mbalimbali ya kitaaluma ambao ni Rick Ngowi, Musa Sultani, Deogratius F. Mkawe, Sr. Rehema Mkundiwe na Furaha J. Masatu. Sambamba na hilo nawashukuru sana wahadhiri wangu wa kozi ya KIS 206 Uandishi wa Kubuni I na KIS 305 Uandishi wa Kubuni II; Mwalimu Eric Ndumbaro na Mwalimu Furaha J. Masatu ambaye nimeshamtaja awali kwa ushauri wao mzuri kuhariri mashairi yangu hakika Mungu awalipe muda wenu mlioutumia na msonge mbele zaidi.  
Niwashukuru kwa dhati wazazi wangu niwapendao Peter Emanuel na Beatrice J. Hamisi, dada zangu Neema Peter na Stela Peter, Kaka zangu Stephano Peter, Yusuph Peter na Daniel Peter kwa kunilea na kunisaidia kwa upendo wao usio kifani hata kuniwezesha kushiriki kutunga mashairi.
Pia shukrani zangu za dhati ziwaendee wahariri na wasomaji prufu wa mashairi yangu walioshirikiana nami katika kukamilisha kazi hii kwa kunitia moyo si rahisi kuwataja kwa majina yao yote lakini wachache ni hawa; Erick Ndumbaro, Furaha J. Masatu, Masanja Jilala, Eston Salvatory, Faki Sheha na Hijiraimu.
Nitakuwa mchoyo wa fadhila nisipowashukuru marafiki na wanafunzi wenzangu wa mwaka wa Chuo Kikuu Cha Kikatoliki Mwenge kwa kozi zote, siwezi kuwataja kwa majina yao yote lakini wachache wao ni pamoja na Masanja Jilala, Damas Meshack, Zengo Michael, Yohana Philemon na Shelly Renatus kwa maoni yao mazuri Mungu awabariki.
                                                                                                         




IKISIRI

Mashairi ya mwalimu Juma ni miongoni mwa zao katika kozi za Uandishi wa kazi bunilizi za fasihi.  Mashairi yanaeleweka kwa wasomaji kwani yametumia lugha inayoeleweka na iliyopikwa vizuri yenye misemo, taswira, matumizi ya picha, tamathali za semi, na mbinu nyingine za kisanaa hivyo inaleta burudani kwa msomaji pindi asomapo.
Mashairi haya yamepikwa vizuri kwa kuitalii miundo mbalimbali ambayo huongoza utunzi wa mashairi kwa kurejelea kanuni za umapokeo kwa kiasi kikubwa kwa kuyasawiri mambo mbalimbali ambayo yako katika jamii hasa kwa kuyafichua na kuielimisha jamii ili iweze kuyaepuka.
Vilevile mashairi haya yanatoa maonyo kadha wa kadha ambayo jamii haina budi kuyapokea ili iweze kuendana na mazingira halisi ya watanzania kwa kuwa na mienendo mizuri, kufanya kazi na kuepuka wimbi la utegemezi pindi watu wanapotafuta maisha kwa lengo la maendeleo binafsi na jamii kwa ujumla wake. Pia mashairi ya mwalimu Juma yanatoa mwanga kwa jamii namna ya kuishi na kuzikabili changamoto mbalimbali zilizopo katika jamii na zinazoyakumba makundi mbalimbali ya watu hasa vijana ambao ndio Taifa la kesho.

Na Mwl Juma.
Visafi vyatamanika, sitiri yake vichafu
Vichafu visopendeka, vile vya kichefuchefu
Chefu yule wake taka, chanzo cha uharibifu
Kiliwacho ni uchafu, sharti yake unawe.
Vyatawanya kila zoni, kumbe navyo ni uchafu
Kunyaka kwazo pupani, mnyako uso faafu
Bila haya uzunguni, ukahamia kwa tifu
Kiliwacho ni uchafu, sharti yake unawe.
Chakula nacho uchafu, sharti yake unawe
Wenye vilemba mfu, vilowabebea mawe
Nje makaburi faafu, ndani yajaa kiwewe
Kisafi nacho kichafu, kama fumo mwenda chini.
Fikrani vyanijia, vile vya kichefuchefu
Nani alopulizia, dawa mjifanye wafu
Zao taka walofia, kufanya urembo mfu
Kisafi nacho kichafu, sharti yake unawe.
Ubongo tujivunie, kama tulo na ubongo
Vya asili jivunie, kwa nguvu kama wabongo
Uzalendo tuenzie, kama tusokunywa gongo
Kichafu kiwe kichafu, tupende uzuri wetu.

CHURA

Na Mwl Juma.
Chura kuishi shirika, ndiyo yao tamaduni
Si shaka yafahamika, ndivyo tangia zamani
Wa jina la kusifika, ndiye chura wa majini
Ukweli wajulikana, kwa miongo na miongo.
Kwa mie yanonijia, katu yaso kawaida
Kuwaza na kuwazua, kiumbe aso na shida
Kwenye mito kuzagaa, maji ni yake faida
Yote haya kawaida, kwa wa jana na wa leo.
Wakaishi kwa furaha, majini vyakula tele
Amani bila karaha, mwendo wa vigelegele
Umoja kwao silaha, katu pasina kelele
Hii yao kawaida, vyura wakazi wenyeji.
Ghafla chura kajawa, yake mambo fikrani
Kutaka kuhama bwawa, kubadili maskani
Hataki kushauriwa, chura yule wa majini
Kweli chura kaamua, atengane na wenzake.
Tarehe ikawadia, yake chura kufungasha
Ugenini kuhamia, nchi kavu karibisha
Taratibu mazoea, mitindo ya kupotosha
Na shughuli kuzifanya, tena nasema haramu.
Si ndoto chura mgeni, ukwasi kujivutia
Magari kwake nyumbani, ngome kuyazungushia
Masikini asilani, dharau kwao kutoa
Hakujua ni masika, kiangazi kinakuja.
Ukame ukawadia, nchi kavu yote jangwa
Na jua likasogea, chura mali zikalengwa
Ardhi kujichimbia, mvua kwake ni lengwa
Ardhi ikachemka, kama moto uwakao.
Kufumba na kufumbua, chura yu jasho mwilini
Tena akishangilia, kwa makofi ardhini
Akilini akijua, mvua i vuruguni
Mwanzo ukawa kwa chura, kuumbuka ugenini.

NGULI WA VICHEKO

Na Mwl Juma.
Kumezuka mashindano, yasobagua jinsia
Yalo pa msongamano, yeyote kutamania
Liso shindano la ngano, vicheko kushindania
Huyu yule achekaye, wa mwisho hucheka sana.
Vikawekwa vichochezi, nia cheko kutokea
Kwa stori za makuzi, tena chuku kuwekea
Cheko zikawapa kazi, haya zikawakimbia
Huyu yule achekaye, wa mwisho hucheka sana.
Pasi kujali u nani, kwako kucheka kuloje
Chekozo zahusu nini, kwakezo zimekomaje
Nacho cha taimu gani, mimosao ‘metekaje
Huyu yule achekaye, wa mwisho hucheka sana.
Washindani mso macho, kuwa kodo mchekapo
Kwani kipo kikulacho, epuka kucheka papo
Hata kiso chakulacho, mwanzo usicheke hapo
Huyu yule achekaye, wa mwisho hucheka sana.
Wa mwisho hucheka sana, epuka kucheka mwazo
Wache wachochee mwana, usijegeuka kenzo
Cheko mwanzo huchoshana, mithili betri chenzo
Huyu yule achekaye, wa mwisho hucheka sana.

BLUUTUTHI

Na Mwl Juma.
Hodi hodi simu janja, mliopo madukani
Ndiyo simu wa viganja, vidole mtelezoni
Wasofichwa kama ganja, wenye hofu ya mbaroni
Simu janja ni ujanja, bluututhi ya nini?
Fikrani kunijia, pawani bluututhi
Kuwaza na kuwazua, utisho uso hadithi
Kunusa chipsi njaa, pasi hati ya urithi
Simu janja ni ujanja, bluututhi ya nini?
Wacha wako uchokozi, kumezea ungo mate
Imekuwa yako kazi, wa mbalini uwanate
Yako kodo waziwazi, mwenye pete yako tete
Simu janja ni ujanja, bluututhi ya nini?
Kufumba na kufumbua, mapono yakawa visa
Dumuzi ukaletea, vinyonyi kwa samakisa
Pawani zote kufia, mithili yake mimosa
Simu janja ni ujanja, bluututhi ya nini?
Langu moya nakuuma, sikioni ung’amue
Bluututhi ya kiyama, vipanya jiepushie
Njia kuu iwe mama, hapa huku zifukie
Simu janja ni ujanja, bluututhi ya nini?

KIJIBA CHA MWITU

Na Mwl Juma.
Binti mwali uso mwali, kwa sie nini wataka
Takozo zisopo tuli, shebeduzi zisonyaka
Mtimako kawa tuli, mahaba huba kutaka
Neema uso na wema, ulo kijiba cha mwitu.
Kinandacho ukateka, mara hisia kudata
Ya kisomoni kutaka, bila furushi la data
Wodi ya jiba kutaka, darasa lenye utata
Neema uso na wema, ulo kijiba cha mwitu.
Sautiyo yawa pingu, kuteka kila hadhira
Takozo milio bangu, walo sumu kukuchora
Kuvimba yao marungu, kupiga alowachora
Neema uso na wema, ulo kijiba cha mwitu.
Punde rungu lipokuja, yake kutimiza kazi
Kajifanya kuyachuja, eti sawa na mzazi
Bohari likayafuja, mbio zilo waziwazi
Neema uso na wema, ulo kijiba cha mwitu.
Kila rungu lipopata, wake mtima kusuza
Lako Ini kujikata, kwa wivu ulo na kiza
Marungu yalokufata, kwayo chuki kuikuza
Neema uso na wema, ulo kijiba cha mwitu.
Langu wazo chukueni, ulompenda mwambiye
Wali ukimya wacheni, zenu haya zikimbiye
Bwangai chuki wacheni, adili wema nduguye
Neema uso na wema, ulo kijiba cha mwitu.

NANI ATOKE!

Na Mwl Juma.
Wetu yehova twaomba, mtukufu yako sifa
Wako viumbe twaimba, sikie nyimbo za sifa
Za mseto na marimba, kama enzi za kayafa
Lugha ndiyo yetu nyenzo, zetu haja kutimiza.
Punde  mola kuifanya, yetu sayari dunia
Kiumbe mtu na panya, na wengine kutokea
Kama mchanga wa sanya, ubaguzi kuzukia
Jipu baya hili bovu, kama fumo mwenda chini.
La fikirisha akili, si kwa yule wala huyu
Kijeba mtu mbigili, uvae pete ya mbuyu
Mawazo yaso adili, kila uchao mabuyu
Nomino yake tatizo, ubwangai yako kazi.
Makundi yaso shirika, yakaundwa ya kisomo
Dhaifu kusaidika, kupata yao kipimo
Nakiri pasina shaka, kisomo kiso kikomo
Kurushiana arafa, za kutegua mitego.
Nawaza na kuwazua, washirika chapuchapu
Pasi shaka jiungia, ya mitandao wasapu
Idadi kujipangia, kuhofia kwa majipu
Mawazoni kunijia, wasapu ya kijamii.
Bila hili wala lile, tangazo wasapu hilo
Alozidi sio yule, kibwangai jasho hilo
Kigugumia si kwele,asipingane na hilo
Kwa huzuni kutamka, basi wa mwisho atoke.
Punde sakata epapu, kumvaa adimini
Kwa kuondoa wasapu, jina pasipo idhini
Kwani kibwangai jipu, kujisafisha ummani
Hili jipu baya bovu, sharti litumbuliwe.

MAKALIO

Na Mwl Juma.
Yatutekenya hisia, Kwa ukubwa makalio
Wapenzicho  kusifia, kuvuta makumbatio
Mwili ganzi kuzimia, yatikisapo milio
Yawe madogo makubwa, huyu yule kujivuna.
Dereva kichwa kuhimwa, mwendo kuingiza gia
Kasi mshale kusomwa, juu ya asilimia
Katu taa kutozimwa, hapa huku jivunia
Yawe madogo makubwa, huyu yule kujivuna.
Mvua kuyasitawisha, kiburi kukuzidiya
Midomo kuitepesha, jiona wakamiliya
Bia zako kuzichosha, kuusambaza umbeya
Yawe madogo makubwa, huyu yule kujivuna.
Makubwa yamegeuka, asali kuwa shubiri
Macho nayo kukodoka, ukame kukushamiri
Madogo kutamanika, katu bohari kukiri
Yawe madogo makubwa, huyu yule kujivuna.
Wengio wamegundua, kweli za yako maisha
Ubwangai twaujua, usiku wajionesha
Madume kuwachekea, garini kujipitisha
Yawe madogo makubwa, huyu yule kujivuna.
Kila dume lakubeba, maradhi jichukulia
Na UKIMWI kuubeba, sababu yako tamaa
Gonjwa lisilo na tiba, nguvu kazi yapotea
Yawe madogo makubwa, huyu yule kujivuna.
Zangu ndugu sikieni, sidate na makalio
Langu somo sikieni, elimu kwenu kioo
Nzuri tabia enzini, kwenu iwe kumbatio
Yawe madogo makubwa, huyu yule kujivuna.

ANUANI YANGU

Na Mwl Juma.
Nina habari muhimu, kwenuni zangu maisha
Sina budi kusalimu, kwa heshima za kutosha
Kwa saluti za adhimu, pasina kumng’unyisha
Heshima kwao wazazi, kunilea tangu kinda.
Kumbukumbu zanijia, tanguzo kinda maskani
Utimamu kunijia, kablapo baleheni
Tisa miaka najua, kwa eskoti shuleni
Makala yangu nomino, maskani julikana.
Nyisanzi tanguzo shule, la kwanza langu darasa
Mwaka sufuri mbilile, pale kati ziso tasa
Alfani mbili ile, omegani tatu hasa
Yangu kodo waziwazi, vidudu kuvifagia.
Chato kwa Magu nikawa, vidudu nikasomea
Pale la tano likawa, darasa nilosomea
Chenjile shule ikawa, Kahama nikahamia
Kakola shule ikawa, langu saba kutimia.
Mwaka ishirini kumi, changu kwanza kidatoni
Miaka minne mumi, nikatimiza foleni
Foleni nilopo mimi, iso mithili ya buni
Ufaulu kunijia, tunu faraja ya wengi.
Julai yangu safari, changu cha tano kusoma
Kwa furaha bila shari, kisomo pasina homa
Langu bohari kukiri, ulofata ukakoma
Maharageyo kwaheri, mwendo wa vigelegele.
Papu neti ikatema, naona matini tepe
Yangu machoni kusoma, mwendo wa barua pepe
Si kama yule wa homa, ilomkata mapepe
Pundeni hodi getini, Makala naye Mwekau.
Zangu jama sikieni, wa Mwekau furahini
Shika yako kisomoni, mithili yake kunguni
Imarisha tamrini, ya nduguze mtihani
Mshike sana elimu, usimwache atoroke.

WAIFII

Na Mwl Juma.
Kumezuka dijitali, tali mithili ya wali
Isozimika kwa chali, moto ule wa ugali
Muwako kama adili, si nduguze wa adili
Hadhi yake simu janja, waifii mdatoni.
Waifii yenye kasi, pasi shaka yake jeti
Jeti iendayo kasi, katu pasina kubeti
Kubeti kwa wasiwasi, simu hofu ya umati
Hadhi yake simu janja, waifii mdatoni.
Mwenye pawa ya ajabu, nani mwenye uthubutu
Uthubutu wa jawabu, jawabu lenye ukutu
Kutu pasina kutubu, waifii wacha butu
Hadhi yake simu janja, waifii mdatoni.
Waifii mdatoni, kudata simu za hadhi
Kusaliti wa tochini, pasi shaka wenye hadhi
Konekiti wa nguvuni, kama mito ya ardhi
Hadhi yake simu janja, waifii mdatoni.
Langu moya nakuwasa, zoea chako kikavu
Kavu mithili ya kasa, kasa mgeni wa kuvu
Yako manyoya usasa, yauwayo kama kuvu
Hadhi yake simu janja, waifii mdatoni.

GEREZA BUBU

Na Mwl Juma.
Kumetokea malezi, malezi yaso baraka
Si ya wawili wazazi, kwa bayana natamka
Watu wenye zao kazi, watoto kuajirika
Mazuri mengi majumba, siri nyingi kufichika.
Wenye vyao kusafiri, sehemu za mashambani
Jitwalia bila shari, mabinti kuwapa fani
Cha ajabu la hatari, si ndoto usingizini
Kazi wasotarajia, pasi ombi kuzifanya.
Si kazi ya masihala, kwa bayana naeleza
Hekalu lake mhola, kwa shuruti kuliuza
Kwa madhumuni mihela, mwajiri kujitanuza
Mazuri mengi majumba, siri nyingi kufichika.
Kwa nyumba wake ulinzi, kama nyuki mzingani
Hujaona tangu enzi, ndoto kupita getini
Katu langoni mlinzi, pia hutomrubuni
Mazuri mengi majumba, siri nyingi kufichika.
Mateso kuendelea, mabinti haki kukosa
Nani wa kuwaokoa, jamani mso na  kosa
Jamii yote dunia, fichua hii ni kansa
Gamba la kasa mkubwa, yule mwenye siri nyingi.
URAIA NCHI MBILI
Na Mwl Juma.
Wetu Mola mtukufu,
Ulo na wema kunjufu
Pendo liso na turufu
 Hapana wa mithiliyo.

Kwako viumbe vikawa
Majini napo vikawa
Nchi na anga vikawa
 kwa matamko vikawa.

Kupendelea ikawa
kufanya mtu ikawa
Dongo kufanya ikawa
Kuyafinyanga tukawa.

Vyote ulotamkia,
Tena pasi kujalia
Maelfu kwa mamia
Majini na nchi pia.

Viliwavyo kagawia
Vya asili nakazia
Viso sumu nasemea
 Bayana natamkia.

Tamko kusainia
Kwa peni isobungua
Andishi lilo wasia
Mtimani kuwekea.

Mwanzo mlo wa adili
Viko wapi vya asili?
Fahiwani nakubali
Ugenini mwakubali.

Maradhi mwajibebesha
Kisukari kwa presha
Vya fati kujikuzisha
Visa mtindo maisha.

PETE ISOVULIKA

Na Mwl Juma.
Pete kito cha thamani, amani kwake moyoni
Isotoka kidoleni, ndiyo pete ya moyoni
Mtima mtulizoni, kwa pete iso rangini
Amani kwake mtimani, pete kito cha thamani.

Jama pete isotoka, nini siri ya kudumu?
Isopenda kupotoka, kama funiko la dumu
Ikadumu kuzunguka, mithili ya gurudumu
Pete kito cha thamani, amani kwake mtimani.
Wakariri chako chanda, usivaliwe kwingine
Majirani walopinda, kachoma kama senene
Zao shingo zikakonda, kutaka zuri unene
Pete kito cha thamani, hakivaliwi kwingine.
Jirani wakumezea, zao kodo kukodoka
Kwa hila kuichukua, wakijua itavika
Pete ikawazibia, lake tundu kuvalika
Pete kito cha thamani, hakivaliwi kwingine.
Na Mwl Juma.
Zamanizo za matenga, yafumwayo kwazo nyasi
Nyasi kusitiri menga, menga isoleta wasi
Wasi kwakezo mkinga, jama mbeba fenesi
Wetu anko tafrani, lakelo tenga ni kwele.
Miongo ‘tano mepita, matenga yayo meona
Meona anko lapwita, matunduye yasobana
Bana makubwa kupita, chini madogo bayana
Wetu anko tafrani, lakelo tenga ni kwele.
Lake anko labagua, mafenesi ilobeba
Beba kubwaga chunjua, kama ndizi za muleba
Leba ya mama kulia, mithili kwayo maleba
Wetu anko tafrani, lakelo tenga ni kwele.
Bila woga kupanua, kwakezo kupe matundu
Tundu lililowaboa, kupita pasina gundu
Gundu liso kubebea, kasoro za seli mundu
Wetu anko tafrani, lakelo tenga ni kwele.
Tengani matundu lango, vigezo umepanua
Panua yake mipango, hofu kufuga kwelea
Kwelea aso maringo, safi hewa kuiua
Wetu anko tafrani, lakelo tenga ni kwele.
Matundu yamechukiwa, si kupe wala kunguni
Nguni hata mbu mekuwa, kukosa keki tengani
Ngani kuwatoa yawa, bila huruma ummani
Wetu anko tafrani, lakelo tenga ni kwele.
Wengio waso tengani, walo sifa za tengani
Ngani kuvuta kwa kani, pasi hongo ya kihuni
Huni mbio za mwituni, furaha mtelezoni
Wetu anko tafrani, lakelo tenga ni kwele.
Tenga la anko mependa, anko pasi shaka Magu
Magu mtu aso kinda, afagiaye magugu
Gugu sugu la kupinda, mithili yakeyo sugu
Wetu anko tafrani, lakelo tenga ni kwele.
Dunia si kama shuka, unayoweza kushika
Sijifanye mhusika, wa dunia Kama shuka
Mabaya kuyatamka, na kwa watu kusikika
Hasidi ubadilike, jaribu kuelimika.
Takonda kwa roho mbaya, na dawa katu haipo
Chuki ni safura piya, tena bila ya malipo
Hakuna wakukulipiya, popote pale ulipo
Yakupasa zingatia, sote ni waja wa mungu.

NYAMA YA ULIMI

Na Mwl Juma.
Wengi wetu mesikia, wasomi wa vitabuni
Vyake dini nakazia, maandiko ya mwangani
Madhambi kuyakemea, kwa shuruti si utani
Yote haya twayajua, hata wale wa mizimu.
Pasi chenga yaeleza, bayana kufafanua
Kiungo chenye kumeza, ulimi sote twajua
Kama njiti ya kumeza, misitu ya Tanzania
Ulimi kitu hatari, pasina pingu huuwa.
Kiumbe usiyejua, kuchagua la kunena
Nani amekugawia, ganja isiwe banana
Ushauri kukataa, nakueleza bayana
Acha wako unafiki, ukinyonga kuuvua.
Ndogo chembe hatari, si wakomavu wadogo
Katu bila tahadhari, huchoma hata magogo
Daktari wake siri, ukimya pasina pigo
Sina budi kuunena, ukweli shubiri chungu.
Kuuweka wako pingu, ulimi bila dhamana
Kuuondoa uchungu, ule wa maji ya kana
Wenye kufunika mbingu, migogoro kutokana
Wekea pingu ulimi, misitu isitoweke.

UTOMVU WA PAPAI

Na Mwl Juma.
Ndugu zangu sikieni, wasia ulo upendo
Pasi shaka pokeeni, wasiani uso fundo
Wabichi wakomaani, meupe maji mrindo
Jama maji tiba sumu, utomvuni mwa papai.
Kwake rangini kufana, mithili yake maziwa
Majini kusonatana, si mgando maziwa
Utomvu maji kulina, yake meupe ni dawa
Jama maji tiba sumu, utomvuni mwa papai.
Utomvuni mwa papai, usokauka shipani
Mithili yake mayai, mwa kaka mzungukoni
Tena yake maji ai, faranga kwake nyumbani
Jama maji tiba sumu, utomvuni mwa papai.
Watumiwa kama dawa, ngozini kuitepesha
Vijidudu kuviuwa, sirosisi kuifisha
Viharusi wafukiwa, makaburi ya kutisha
Jama maji tiba sumu, utomvuni mwa papai.
Utomvuni tiba sumu, pasi huruma huvuma
Mithili yake kisumu, dawa vitambi vya zama
Kufa kwake kuvu sumu, mithili yake ukoma
Jama maji tiba sumu, utomvuni mwa papai.
Wangu wasia utomvu, ule wa maji meupe
Upakwao kwa mashavu, kwa mapozi ya utepe
Wabichi kwa wakomavu, mwe makini na meupe
Jama maji tiba sumu, utomvuni mwa papai.
TAARIFA MUHIMU KUHUSU MWANDISHI
Juma Peter alizaliwa tarehe 20 mwezi Desemba mwaka wa 1993 katika Wilaya ya Iramba Mkoani Singida na baadaye kupata Elimu katika shule ya Msingi Nyisanzi iliyopo Wilaya ya Chato Mkoani Geita kuanzia mwaka 2003-2007, ndipo alihamia Shule ya Msingi Kakola “A” iliyopo Wilaya ya Kahama Mkoani Shinyanga 2007-2009. Baadaye alijiunga na Elimu ya Sekondari katika shule ya Sekondari Bulyanhulu iliyopo wilayani Kahama mkoa wa Shinyanga na kutunukiwa Certificate of Secondary Education Examination (CSEE) 2010-2013. Mwalimu Juma Peter alifaulu mtihani ya kidato cha Nne na kufanikiwa kuendelea na masomo ya kidato cha Tano na Sita katika shule ya Sekondari Itigi iliyopo Wilaya ya Manyoni mkoani Singida katika Mchepuo wa HGK na kutunukiwa cheti cha kuhitimu kidato cha Sita yaani Advanced Certificate of Secondary Education Examination (ACSEE) 2014-2016. Badaye alifaulu mitihani yake ya kidato cha Sita na mwezi Oktoba 2016 alifanikiwa kuchaguliwa kujiunga na Elimu ya Chuo Kikuu katika Chuo Kikuu Cha Kikatoliki Mwenge kilichopo Wilaya ya Moshi mkoani Kilimanjaro kusomea Shahada ya Kwanza ya Elimu Sanaa yaani Bachelor of Education in Arts (Jiografia na Kiswahili).



No comments

Theme images by jangeltun. Powered by Blogger.