NAMNA YA KUJITENGENEZEA MTANDAO WA WATU WANAOKUAMINI


NAMNA YA KUJITENGENEZEA MTANDAO WA WATU WANAOKUAMINI
Na Mwl. Juma
Rununu: +255762957992
Moshi-Tanzania

Tunaishi kwenye zama ambazo mtu kuwa na kundi kubwa la marafiki kwenye mitandao ya kijamii inachukuliwa kuwa mafanikio. Mahusiano haya ya mitandaoni hata hivyo ni nadra kuleta tija kwenye maisha halisi. Ndio kusema, umuhimu umuhimu wake unabaki kuwa kwenye matangazo ya biashara, kubadilishana taarifa kupitia arafa, mawasiliano sikizi ama vionwa na shughuli zingine zisizohusisha mahusiano ya karibu baina ya watu.
Kwa upande mwingine, tunafahamu kuwa mafanikio yetu kibiashara, kazini na katika maisha kwa ujumla yanategemea kiwango cha ukaribu tunaoujenga na watu na watu na si idadi ya watu tunaofahamiana nao. Namna gani tunaweza kuaminika na watu wanaofahamiana nao na hivyo kujenga mtandao wa watu tunaoweza kuwategemea ni ujuzi tunaouhitaji.
MBINU (05) MUHIMU ZINAZOWEZA KUKUSAIDIA KUJENGA MTANDAO WA WATU WANAOKUAMINI
Hapa ninakuonesha mbinu tano (05) muhimu zinazoweza kukusaidia kujenga mtandao imara na watu.
  1. Lenga kundi mahususi la watu
Unataka kuwa karibu na watu wa kundi gani? Unalenga watu unaoweza kujifunza kwao, waajiri, wafanyakazi, wenzako, wateja, watu uliowahi kusoma nao, watu uliowahi kufanya nao kazi au watu wenye taaluma fulani?
Tengeneza orodha ya watu wachache wanaokidhi malengo yako kisha hakikisha unawasiliana nao mara kwa mara. Unapowatafuta usiishie kusema “nilikuwa nakujulia hali hali tu” bali nenda mbele kufahamu wanapendelea nini, vitu gani vinawagusa zaidi na shughuli gani wanaipatia uzito zaidi. Hata hivyo, katika kuwasiliana nao epuka kuonekana wewe ni mtu usiye na shughuli unayepotezea watu muda.
Pia unaweza kuwa na kundi lingine dogo la watu ambao pengine huwahitaji kwa saa lakini wanaweza kuwa msaada mkubwa huko uendako. Hawa wanaweza kuwa watu waliopo kwenye ofisi mbalimbali za umma, jiwekee utaratibu wa kuwasiliana nao mara kwa mara. Tumia WhatsApp, SMS, mitandao ya kijamii kufanya mawasiliano nao hata kwa mambo ya kawaida.
  1. Jifunze kuwasiliana na watu
Watu wengi hatujui nguvu ya mazungumzo tunapokuwa na watu. Hatujui siri ya kugusa mioyo ya watu tunapozungumza nao. Unaonana na mtu lakini huonekani kuheshimu muda wa mtu unayezungumza naye.
Mtu anaongea wakati huo huo anahangaika kushika shika simu, haoneshi uzingativu, hachangamki lakini bado anashangaa inakuwaje watu hawaendelezi mawasiliano baada ya kuachana naye.
Ikiwa unataka watu wavutiwe na wewe na watamani kuendeleza ukaribu na wewe, jifunze mbinu za mawasiliano. Unapokutana na mtu, kwa mfano, changamka, tabasamu, itikia vizuri kile anachokizungumza mtu, ongea kwa ujasiri, uliza maswali ya maana na pia jibu maswali kwa ufasaha. Unapofanya hivi unaongeza uwezekano wa kujenga mahusiano ya kudumu.
  1. Wafanye watu watamani kukufahamu
Mojawapo ya mambo yatakayoongeza uwezekano wa watu kuendeleza ukaribu na wewe ni uwezo wako wa kuwafanya watu wakudadisi kwa lengo la kukufahamu zaidi. Usifanye kosa la kumfanya mtu akiachana na wewe awe amechoka na asiwe na shauku ya kukutana na wewe tena.
Kuongea sana, kujisifu, kulalamika, kuwasema watu ni baadhi ya tabia zinazoweza kumfanya mtu makini asitamani kukutana na wewe tena. Ukitaka kujenga udadisi wekeza kwenye maarifa na ujuzi adimu. Jifunze mambo kwa kina kwenye eneo lako la utaalamu, bobea kwenye kitu na uhakikishe unakijua kwa kina chake.
Unapopata nafasi ya kuzungumza, usifanye kosa la kuonesha unababaisha mambo kijuu juu. Tumia fursa vizuri kuthibitisha kuwa una kitu cha tofauti ndani yako na kwamba mtu akiwa karibu na wewe kuna kitu atakifaidi. Huwezi kusahaulika.
  1. Usisubiri uwe na shida ndipo uwatafute watu
Jifunze kumwagilia mtandao wako hata kabla hujaanza kuuhitaji. Wafanye unaowafahamu wawe sehemu ya maisha yako na wasikuone kama mzigo. Hakuna mtu angependa kuwa karibu na mzigo utakaomchelewesha kwenda kule aendako.
Usiwatafute watu pale tu unapokuwa na shida. Usiwe mtu wa kukopa kopa bila sababu. Kumbuka kila anayekusaidia anapunguza wajibu wake kwako. Utakapomtafuta siku nyingine wakati wa shida anaweza kukukatalia kwa ujasiri kwa sababu humdai fadhila.
Jifunze kula na kipofu, wakumbuke watu hata kwenye nyakati ambazo huonekani kuwa na shida. Kama umeajiriwa wakaribishe watu wako kwenye shughuli zinazohusu kazi. Ikiwa kuna mikutano inayokaribisha watu kutoka nje ya taasisi tumia fursa hiyo kuwaita watu wako.
  1. Tafuta fursa za kuwasaidia watu
Kanuni rahisi kwenye maisha ni kuwasaidia watu kabla hujatarajia wakusaidie wewe. Jifunze watu wako wa karibu wanahitaji msaada upi na jitahidi usaidie. Unaposikia mtu unayemfahamu amepatwa na matatizo usisubiri uombwe msaada. Changamkia matatizo ya watu kwa kutumia uwezo wowote mdogo ulionao.
Unapofanya hivyo unawafanya watu wakuone kama mtu wa msaada anayeweza pia kutegemewa katika nyakati fulani. Kwa namna hii unavuta watu kwako na haitakuwa rahisi wapuuze pale utakapohitaji msaada wao.
DONDOO ZA AJIRA NA KAZI
Kwa nini unahitaji mtandao wa ajira (Networking)?
  1. Mtandao ni sawa na mbegu iliyopandwa ili kesho ama keshokutwa ikusaidie. Mtandao unaojengwa kwa kuwasaidia wengine unakuwekea mazingira ya wewe mwenyewe kusaidiwa siku moja.
  2. Mtandao unaweza kuwa chanzo muhimu cha taarifa zinazohusu nafasi za kazi. Hata kama una kazi tayari unapofahamiana na watu wa kada fulani inaweza kuwa rahisi wewe kupata ajira uipendayo.
  3. Kupitia mahusiano na watu wako wa karibu unaweza kuwa na watu wanaokuhamasisha kupiga hatua moja mbele. Wakati mwingine heshima yako inategemea aina ya watu unaoonekana nao.
  4. Mtandao unakujengea marafiki unaoweza kuwasaidia pale unapoweza. Unapotoa msaada kwa mtu nafsi yako inapata utoshelevu.

No comments

Theme images by jangeltun. Powered by Blogger.